Abstract:
Utafiti uliofanyika ulikuwa na lengo la jumla la kuchunguza mchango wa TEHAMA katika
ufundishaji na ujifunzaji wa stadi ya kuzungumza katika lugha ya Kiswahili kwa wanafunzi wa
shule za sekondari teule wilayani Nyamasheke nchini Rwanda. Malengo mahususi ya utafiti
yalikuwa mawili. Kwanza, kubainisha nafasi ya TEHAMA katika ufundishaji na ujifunzaji wa
stadi ya kuzungumza Kiswahili kwa wanafunzi wa shule za sekondari teule wilayani
Nyamasheke nchini Rwanda. Pili, kuunda miongozo ya utumiaji wa TEHAMA katika kuboresha
ufundishaji na ujifunzaji wa stadi ya kuzungumza Kiswahili kwa wanafunzi wa shule za
sekondari teule wilayani Nyamasheke nchini Rwanda. Kwa kutimiza malengo haya, utafiti
uliegemezwa katika Nadharia ya Kuunganishwa. Wango la utafiti lilihusisha wakurugenzi,
wakuu wa masomo, wanafunzi na walimu katika shule za sekondari teule wilayani Nyamasheke.
Sampuli ya utafiti ilihusisha wanafunzi 115 wa kidato cha sita. Wanafunzi hawa waliteuliwa kwa
makusudi kwa kuwa ndio ambao wana umahiri katika Kiswahili ukilinganisha na wanafunzi wa
vidato vya chini. Aidha, sampuli ilihusisha walimu 5, wakurugenzi 5 na wakuu wa masomo 5
ambao waliteuliwa kwa kutumia usambulishaji lengwa. Ili kukusanya data, mbinu za usaili,
uchambuzi matini na ushuhudiaji zilitumiwa. Aidha, matokeo ya utafiti yamebainisha kwamba
TEHAMA ina nafasi kubwa katika ufundishaji na ujifunzaji wa stadi za kuzungumza Kiswahili.
Kwanza, TEHAMA hurahisisha ufundishaji na ujifunzaji wa stadi za kuzungumza. Pili,
TEHAMA inawezesha walimu na wanafunzi wa lugha kupata zana za kisasa za kufundishia stadi
za kuzungumza. Tatu, TEHAMA ina nafasi katika kuongeza hamasa ya kuzungumza Kiswahili
miongoni mwa wanafunzi. Nne, TEHAMA inatumiwa ili kuwezesha wanafunzi kuwasiliana na
wazawa wa Kiswahili kwa urahisi. Hata hivyo, matokeo yanaonesha changamoto katika
matumizi ya TEHAMA, ikiwa ni pamoja na uhaba wa zana za TEHAMA na ukosefu wa ujuzi
wa kutumia programu za TEHAMA. Ili kuepukana na changamoto hizi, tunapendekeza kuandaa
semina kwa walimu wa Kiswahili, kupanga ratiba ya matumizi ya chumba cha kompyuta,
kuongeza zana za TEHAMA kwa ajili ya kufundisha stadi za kuzungumza Kiswahili. Mwisho,
utafiti umetoa miongozo ya utumiaji wa michezo ya KiTEHAMA na mikutano ya video
mtandaoni na utumiaji wa programu za mtandaoni za kufundishia na kujifunzia stadi za
kuzungumza Kiswahili.